TIMU ya Singida imeimarisha
safu yake ya ulinzi kwa kumsajili beki wa Mghana, Malik Antri ambaye alikuwemo
kwenye kikosi cha timu ya taifa ya wachezaji wa nyumbani kwa ajili ya michuano
ya CHAN.
Taarifa ya Mkurugenzi wa Singida United, Sanga Festo imesema kwamba
Antri amekwishawasili nchini tayari kuitumikia Singida United ambayo inapambana
kuhakikisha inatwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara katika msimu
wa kwanza tangu wapande.
Amesema kwamba Antri anachukua nafasi ya Elisha Muroiwa
aliyerejea kwao Zimbabwe kufuatia matatizo ya kifamilia yanayomsumbua.
Antri anakuwa mchezaji wa nane kusajiliwa dirisha dogo Singida
United, baada ya washambuliaji Daniel Lyanga kutoka Fanja ya Oman, Kambale
Salita 'Papy Kambale' kutoka Etincelles ya Rwanda na Lubinda Mundia kwa mkopo
kutoka Res Arrows ya Zambia.
Wengine ni chipukizi Issa Makamba, Assad Juma, Ally Ng’azi na Mohamed
Abdallah waliokuwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya vijana ya Tanzania chini
ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys kilichoshiriki fainali za U-17 Afrika
nchini Gabon Mei mwaka huu.
Singida United inayofundishwa na kocha wa zamani wa Yanga, Mholanzi Hans
van der Pluijm kwa sasa inashika nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa
na pointi 20 baada ya kucheza mechi 11.
Singida inazidiwa pointi tatu na Simba na Azam na mbili na mabingwa watetezi,
Yanga. Na baada ya mapumziko ya wiki tatu kupisha michuano ya CECAFA
Challenge Singida itawafuata Njombe Mji FC Desemba 31 Uwanja wa Saba
Saba huko Njombe, mchezo utakaoanza Saa 8:00 mchana.
No comments:
Post a Comment