
Na. Immaculate Makilika, MAELEZO. DSM....
Utafiti ulofanywa mwaka 2009 na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa masuala ya watoto hapa nchini ulionyesha kuwa kuna kiwango kikubwa cha ukatili dhidi ya watoto.
Hata hivyo, pamoja na kuwa ni utamaduni wa kigeni kuripoti matukio mbalimbali kupitia namba za simu na kwenye mitandao, matumizi ya namba 116 (Child helpline) hapa nchini yamesaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa taarifa za ukatili dhidi ya watoto.
Kama anavyoeleza Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Mtoto kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Bwana. Benedict Missari kuanzia mwezi Juni 2013 hadi mwezi Juni 2014, Wizara hiyo ilipokea jumla ya simu 16000 kati ya hizo1659 zilielezea ukatili dhidi ya watoto.
Kati ya simu hizo 1659, “simu 107 zilikuwa za ‘physical violence’, 23 za ubakaji, 23 za unyanyasaji mwingine wa kingono, 69 ni za kutelekezwa, 6 za utekwaji wa watoto, 12 zilihusu mimba kwa watoto huku 21 ni za uuzwaji wa watoto kwenda maeneo mbalimbali mfano Zanzibar na nchi za Uarabuni”.
Watoto walio na umri wa chini ya miaka 18 nchini Tanzania ni sawa na asilimia 51 ya jumla ya idadi ya wananchi wote nchini.
Ili kukabiliana na hali hiyo, mnamo tarehe 3 Januari, 2013 Serikali chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na Asasi isiyokuwa ya Kiserikali ya C-Sema chini ya Child Helpline International(CHI) ilianzisha na kuendesha mtandao wa mawasiliano ya simu katika maeneo ya majaribio (Pilot Areas) katika wilaya sita ambazo ni Wilaya/Manispaa za Temeke, Magu, Bukoba Vijijini, Musoma Mjini, Kasulu na Hai ili kupata taarifa za ukatili wa watoto kwa kupiga simu bure kwa kutumia namba 116(Child helpline).
Mtandao huo wa mawasiliano unatoa fursa kwa watoto na au watu wazima kwa niaba ya watoto kutoa taarifa za ukatili unaofanywa kwa watoto katika eneo fulani ili kuwezesha wahusika kufuatilia kwa karibu na kutoa msaada kwa mtoto/watoto waliofanyiwa vitendo vya ukatili kwa kuwachukulia hatua wahusika wa vitendo hivyo vya ukatili.
Kupokelewa kwa taarifa ukatili dhidi ya watoto kumeweza kufanyiwa kazi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo makampuni ya simu kwa kumwezesha mtoa taarifa kupiga simu hiyo bure, Polisi kwenda kukamata wahusika na kuwafikisha sehemu husika kulingana na Sheria na taratibu za nchi, na hospitali kutoa huduma kwa wahusika wa matatizo mbalimbali yanayohitaji huduma za kiafya.
No comments:
Post a Comment