Naibu
Waziri wa Afya, Dk Hamis Kigwangalla (pichani) amewasimamishwa kazi wauguzi sita katika
hospitali ya Temeke kwa kosa la kuomba rushwa.
Wauguzi waliosimamishwa ni Hadija
Salum, Beatrice Temba, Agnes Mwampashe, Elizabeth Mwilawa, Mariam Mohamed na
Marion Said, ambao walikuwa zamu katika wodi ya wajawazito wakati wa tukio
hilo.
“Nimewasimamisha kazi
wauguzi wote waliokuwa zamu jana (juzi) asubuhi, nakuagiza Msajili wa Baraza la
Wauguzi uwasimamishe hadi utakapowasafisha kupitia kamati ya msajili,” alisema Dk
Kigwangalla.
Mmoja wa wajawazito, Loshan Seif
alisema alipowasili juzi asubuhi kwa ajili ya kujifungua, muuguzi mmoja wa zamu
alimtaka kulipia Sh5,000 za gloves.
“Siku zote huwa
natumia bima lakini jana (juzi) wakaniambia hawatumii, nitoe Sh5,000 za gloves,
baadaye niliambiwa natakiwa kuwa na uzi wa mshono, sindano na vingine hivyo
kama sina nitoe fedha,” Alisema Seif.
Dk Kigwangalla alifanya ziara ya
ghafla hospitalini hapo jana saa 9.00 alasiri.
Akizungumza jana alasiri baada ya
kufanya ziara ya ghafla Hospitalini hapo na kupata malalamiko hayo kutoka kwa
wanawake waliojifungua.
“Mama anaambiwa atoe
fedha ya gloves Sh5,000 wakati dukani zinauzwa Sh1,000, nataka liwe fundisho
kwa wote wanaotuongezea vifo vya wajawazito kwa tamaa ndogondogo,” alisema Kigwangalla.
Katika ziara hiyo, Dk Kigwangalla
alishuhudia ubovu wa vyumba viwili vya upasuaji na kutoa maelekezo kwamba,
virekebishwe ndani ya miezi sita.
“Hali ni mbaya ndani
ya hizi ‘theater’ zote mbili zifanyiwe ukarabati iwapo itashindikana
nitazifunga, lazima ziwe na hadhi yake na nitakuja kukagua,” alisema.
No comments:
Post a Comment