Watu wanaoishi na
Virusi vya Ukimwi (VVU) mkoani Tanga wametakiwa kuachana na kasumba za kukimbia
kwa waganga wa kienyeji na kuendelea na utaratibu walipangiwa na wahudumu
wa afya wa kutumia dawa kwani hali hiyo inaweza kuwasababishia matatizo
makubwa.
Hayo yalisemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt Asha Mahita (Pichani) wakati
akifungua warsha ya kuwajengea uwezo Waviu washauri ili waweze kuunganisha
jamii kwenda katika vituo vya afya. Warsha hiyo inaratibiwa na Shirika la
AGPAHI mkoani hapa.
Alisema vitendo vya wagonjwa kuacha dawa vinaweza kuwaweka kwenye
wakati mgumu ikiwemo kupata usugu ambao unaweza kupelekea kupoteza maisha
kutokana na kushindwa kufuata utaratibu uliowekwa na kuwataka kuondokana na
tabia za namna hiyo.
“Kuna tabia ambayo imejengeka baadhi ya wagonjwa kuacha kutumia dawa na
kukimbilia kwa waganga wa kienyeji kwani wanapoacha kutumia dozi na kutumia
dawa nyingine.. virusi vinakuwa na usugu hali inayowasababishia hali mbaya
zaidi na hata uwezekano wa kupoteza maisha “Alisema.
“Mpaka watu watambue kuwa hakuna dawa iliyothibitishwa kutibu VVU hivyo
waendelea kuzitumia dawa za kupunguza makali ya VUU (ARV) ikiwemo kuacha kwenda
kwa waganga wa kinyeji kwani wanaweza kukumbana na matatizo makubwa sana
“Alisema.
Aidha alisema pia katika mpango wa mkoa wa Tanga wataendelea
kuhamasisha wananchi kwenda kwenye vituo vya afya ili waweze kujua afya zao
ikiwemo kuweza kuchukua hatua iwapo watabainika wameathirika.
“Lakini pia kwa watoto maana upimaji wao upo chini ikiwemo kuhakikisha
watoto wanaopata maambuzi wanaanzishiwa dawa mapema kwani zitawasaidia kuongeza
maisha yao na kuishi na afya njema”Alisema.
Awali akizungumza katika semina hiyo,Afisa Mradi Huduma Unganishi wa
Jamii wa Shirika la AGPAHI mkoani Geita Richard Kambarangwe alisema warsha hiyo
ni kuwapa elimu zaidi Waviu washauri wanaosaidia kutoa huduma katika vituo vya
tiba na matunzo (CTC) kwa watu wanaoishi na VVU.
Alisema pia kuweza kuwasaidia kupata ujuzi zaidi ili kujifunza mbinu za
kuwatafuta na kuwaunganisha wateja wa CTC na vituo kwa jamii kuweza kupunguza
idadi ya kupotea kwa wateja.
“Lakini pia takwimu za Tanzania na mkoa inaonyesha watu wengi
wanaotumia dawa za kupunguza makali ya VVU wanaweza kupotea kwenye huduma hivyo
shirika la AGPAHI mara kwa mara linazingatia kutoa elimu itakayowasaidia
watu kupata uelewa wa lishe na matumizi sahihi ya dawa “Alisema.
No comments:
Post a Comment