![]() |
Mhe Waziri akimkabidhi Kitambulisho chake mmoja wa
wananchi wa Kata ya Songea Bwana Hassan Ally Shomari wakati wa zoezi la ugawaji
Vitambulisho kwenye sherehe za uzinduzi wa zoezi la Usajili kwa mkoa wa Ruvuma.
Jumla ya Vitambulisho 3470 viligawanywa kwa wanachi wakati wa sherehe hizo.
|
Kaimu
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) Ndg Andrew W.
Massawe ameitaja mikoa ya Mara, Arusha, Iringa, Geita, Lindi, Simiyu, Mbeya na
Songwe kuwa mikoa inayoongoza katika zoezi la kuwasajili wananchi kupata
Vitambulisho vya Taifa; huku mikoa mingine ikiwa nyuma kiusajili kulinganisha
na malengo waliyowekewa.
Akizungumza katika sherehe za uzinduzi wa zoezi la usajili kwa mkoa wa
Ruvuma lilofanyika katika viwanja vya Lisaboni-Songea, Ndugu Massawe amemuomba
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Nchemba kusaidia kuweka msukumo
kwa viongozi na wananchi kwenye mikoa ambayo haifanyi vizuri ili iongeze kasi
ya usajili kwa lengo la kukamilisha usajili kwenye mikoa yao kwa muda
uliopangwa.
Akihutubia wananchi wa Ruvuma waliofurika kwenye viwanja vya Lisaboni
vilivyopo nje kidogo ya mji wa Songea, Waziri wa Mambo wa Ndani ya Nchi Mhe.Dkt
Mwigulu Lameck Nchemba amewasisitizia wananchi kujitokeza kwa wingi kusajiliwa
kwani kuwa na kitambulisho cha Taifa siyo suala la hiyari ni wajibu kwa kila
Mtanzania mwenye sifa kuwa nacho.
“ Mhe. Rais wetu ametoa hela za kuwasajili, zoezi ni bure bado
kujisajiliwa kwenda kupigwa picha na kuchuliwa alama za vidole ikushinde?”
aliuliza Waziri huyo mwenye dhamana kubwa katika kusimamia utekelezaji wa zoezi
hilo.
Aidha amewataka viongozi wa Mikoa na wote wenye dhamana katika
kusimamia zoezi hili kuhakikisha wanashirikiana kwa karibu na Mamlaka ya
Vitambulisho vya Taifa katika kuhakikisha wananchi wenye sifa wanasajiliwa na
kamwe pasiwepo wageni watakaojipenyeza kusajiliwa Vitambulisho vya Taifa kama
raia.
“Kwakuwa NIDA inatoa vitambulisho vya aina tatu, cha Raia, Mgeni na
Mkimbizi basi niwaombe wageni badala ya kufanya udanganyifu wajisajili kwa
hadhi yao kwani siyo dhamira ya Serikali kumfukuza yeyote lakini kuwatambua
Raia wake kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani” alisema
Naye Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe. Christina Mndeme amemhakikishia Mhe.
Waziri mkoa wake uko tayari kusimamia na kuhakikisha wananchi wote wenye sifa
wanasajiliwa na kupata Vitambulisho ndani ya muda uliopangwa na kwamba kamwe
hata mvumilia mtu yeyote ambaye atakuwa kikwazo katika utekelezaji wa zoezi
hilo kwa wananchi; akiwakemea wanasiasa kuingiza siasa kwenye zoezi la Usajili
wananchi vitambulisho vya Taifa.
Mkoa wa Ruvuma wenye Wilaya 5 unakisiwa utawasajili zaidi ya wananchi
900,000 katika zoezi lililopangwa kumalizika ndani ya miezi mitatu. Tayari NIDA
imekamilisha usambazaji wa vifaa na kutoa mafunzo kwa maafisa ambao watatumika
kuwasajili wananchi wa Ruvuma na viunga vyake.
Mikoa mingine inayoendelea na Usajili kwa sasa ni Iringa, Mbeya,
Njombe, Singida, Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Mwanza, Shinyanga, Geita,
Simiyu, Mara, Songwe, Lindi na Mtwara.
No comments:
Post a Comment